Ni siku nyingine mpenzi msomaji wa safu hii ya kona ya
wajasiriamali tunapokutana tena. Karibu katika kona ya wajasiriamali
yenye maudhui ya kuona namna bora ambazo wajasiriamali wanaweza
kuzitumia ili kuendeleza biashara zao na kupata mafanikio.
Sina budi kuwashukuru wasomaji wa kona hii ambao wamekuwa
wakiwasiliana nami juu ya kutafuta namna bora ya kuweza kujenga ustawi
katika shughuli zao. Nawashukuru sana kwa kunitia moyo kuwa tuko pamoja
na mnafurahi kile mnachokipata.
Siku zinayoyoma na sasa ni mwezi wa sita, ambao unatuweka katika
nusu ya kwanza ya mwaka huu wa 2015. Leo katika kona hii ya ujasiriamali
tutakumbushana juu ya baadhi ya makosa ya kuyaepuka ili biashara yako
iweze kupiga hatua.
Mwenye kujua kama unataka mafanikio katika biashara ama la, ni wewe
mwenyewe, kaa chini na utafakari baadhi ya mambo ambayo yanaweza kuwa
kikwazo cha wewe kupiga hatua. Kumbuka unapaswa kudhibiti mambo yote
ambayo yako ndani ya uwezo wako.
Kumbuka ndugu mjasiriamali tunaishi katika ulimwengu wenye mambo
yanayobadilika kila siku. Bila kujituma na kufanya kazi kwa bidii na
kukabiliana vema na changamoto mbalimbali, huwezi kufikia ndoto zako
unazotamani kuzifikia vema, huwezi kupiga hatua.
Mjasiriamali ukiwa na kiu ya mafanikio unahitaji kuamka tena bila
kukata tamaa kwani bado una nafasi. Ili kuepuka matatizo ya kushindwa
katika biashara, hakikisha baadhi ya makosa kama uliwahi kuyafanya
katika kipindi cha mwaka jana huyafanyi tena.
Amini unaweza
Kosa la kwanza, epuka kutojiamini. Vipi tangu mwaka huu wa 2015
umeanza mpaka sasa je, umeweza kujiamini wewe mwenyewe ? Kama hukuweza
kujiamini unafikiri nani atakuamini ? Hakikisha ndugu mjasiriamali
unakuwa mtu wa kujiamini siku zote.
Kumbuka ndugu mjasiriamali kwamba kujiamini kwako kutakupa nguvu ya
kufikia yale unayotamani, kujiamini kwako kutakuwezesha wewe kuwa na
mtazamo chanya (positive attitude) kwa yote unayofanya na kukupeleka
kwenye njia ya mafanikio unayotamani.
Amini kwamba unaweza kufanya vizuri hicho ambacho umeamua kukifanya
na kitakukomboa. Kama mjasiriamali mwenye kiu ya mafanikio, unahitaji
kusema unaweza kwa kila unachofanya, kwani kama wengine waliweza kwanini
wewe useme huwezi?
Jitoe kwa moyo wote
Kosa la pili, kutoweza kujitoa (lack of commitment). Ili kuweza
kufikia mafanikio ya kweli huna budi kujitoa kwa moyo wote pamoja na
kukaa chini na kujiwekea mipango yako mbalimbali. Huna budi kujitoa,
kama huwezi ni vigumu kufanikiwa.
Mafanikio katika ujasiriamali si suala la kulala na kuamka,
unahitaji kujitoa kwa moyo wako wote na akili yako ili mambo yaende.
Usione wajasiriamali wakubwa unaowafahamu wamefanikiwa ukafikiri kuna
njia ya mkato, unahitaji kubadilika.
Kuwa mtu wa vitendo
Kosa la tatu, kutokuwa mtu wa vitendo. Hili ni moja kati ya makosa
makubwa yanayofanywa na wajasiriamali wengi. Inawezekana tangu mwaka huu
wa 2015 umeanza ulikuwa na mipango mingi lakini mpaka sasa ni michache
uliyoweza kuifanya.
Jiulize katika mipango uliyokuwa nayo ni ipi uliitekeleza na ipi
uliiacha, ni wakati wa kujiuliza kwanini hukufanya kile ulichopanga?
Wapo wajasiriamali ambao wamekuwa wazuri zaidi katika kuongea kuliko
kutenda, je, wewe unajiweka katika upande gani?
Ni wakati wa kuamka na kubadilisha mwenendo huo, kuwa mtu wa
vitendo acha porojo. Kuna wajasiriamali ambao wakikuambia mipango yao
unaweza kusema jamaa sasa hivi anakuwa milionea, lakini kuleta mipango
katika uhalisia huwa jambo gumu kwao.
Usifuate mkumbo
Kosa la nne, kufuata mkumbo. Watu wengi wameingia kwenye
ujasiriamali kwa kufuata mkumbo hasa kwa kuiga kutoka kwa wenzao yale
wanayofanya. Wapo ambao kwa mfano wameingia kwenye biashara ya nguo kwa
kuona tu wenzao wanafanya hivyo.
Unapoamua kuingia kwenye ujasiriamali lazima upate msukumo wa ndani
wa wewe kufanya hivyo, hata kama unaiga basi usiige kila kitu kwani
kila mjasiriamali anahitaji kutafuta fursa za yeye kuweza kujenga msingi
wa mafanikio kwa kusimama mwenyewe.
Hivyo yafaa kujiuliza, kwanini umeamua kufanya hicho unachofanya?
Unaweza ukawa kila wakati unalia kwamba hupati mafanikio katika hicho
unachofanya kumbe sababu kubwa ya wewe kutopata mafanikio ni kuingia
kwenye uwanja ambao si wako.
Una mipango gani?
Kosa la tano, kutokuwa na mipango (no planning). Kuna msemo
unaosema "kushindwa kupanga ni kupanga kushindwa". Kama huwezi kujua
unaelekea wapi huwezi kufika huko, ni muhimu kuwa na mipango ili kuwa na
mwelekeo wenye kueleweka na kufaa.
Tunapozungumzia kuwa na mipango yafaa kukumbuka wakati wote sifa za
mipango wajasiriamali wanayopaswa kuwa nayo. Yafaa kuwa na mipango
maalum, inayotekelezeka, inayopimika na kufikika katika muda
utakaojiwekea.
Wajasiriamali wengi huja na mipango ambayo iko juu ya uwezo wao na
hata utekelezaji wake huwa mgumu. Yafaa mipango ya wajasiriamali iendane
na uhalisia na uwezo walio nao katika kuendesha shughuli zao,
vinginevyo watakuwa na mambo yasiyotekelezeka.
Nenda na wakati.
Kosa la sita, kutokwenda na wakati. Tunapozungumzia kwenda na
wakati maana yake mjasiriamali huna budi kubadilika kutokana na
mazingira uliyo nayo. Dunia ya leo si dunia ya jana, dunia imekuwa
kijiji mambo yamebadilika huna budi nawe kubadilika.
Mjasiriamali lazima ujifunze kubadilika kutokana na mabadiliko
mbalimbali katika ulimwengu wa biashara. Ni hatari kufanya mambo
kimazoea kwa kuwa tu yale uliyokuwa unayafanya na kufanikiwa yataendelea
hivyo hivyo, kila siku sio Ijumaa.
Kama unavyoelewa kuna mabadiliko mengi katika dunia ya ujasiriamali
kama vile ya ushindani wa kibiashara, teknolojia na mengine mengi.
Epuka kufanya mambo kimazoea kwa kuhakikisha unajichanganya na kwenda na
wakati. Usijifungie vioo.
Jikune mkono unapofika
Kosa la saba, mpangilio usiofaa wa mitaji ( insufficient funding).
Kuna msemo wa kiswahili usemao, mgongo hujikuna pale mkono unapofika. Na
ndivyo wajasiriamali hufanya kosa hili la kupenda kufanya mambo makubwa
bila kuwa na uwezo wa kutosha.
Wajasiriamali wengi hulia juu ya ukosefu wa mitaji katika
kuendeleza au kukuza biashara zao, lakini pia wapo ambao hupenda kufanya
mambo ambayo hayaendani na hali halisi ya mitaji waliyonayo, hupenda
kufanya mambo kwa kutafuta mafanikio ya haraka.
Inashauriwa ndugu mjasiriamali kujipanga kutokana na uwezo ulio nao
na si kuota ndoto za mchana. Wapo ambao wangeweza kufanya vizuri kwenye
mambo madogo lakini kwa kutaka mafanikio ya haraka wamejiingiza kwenye
biashara zenye mahitaji makubwa.
Kubali hali halisi ya uwezo ulionao na amini kuwa unaweza kufanya
mambo madogo kulingana na mtaji na kidogo kidogo utasonga mbele na
kukua. Kuna baadhi ya biashara unaweza kufanyia nyumbani kwanza bila
kuwa na 'fremu', tafakari hilo na chukua hatua sasa.
Pokea changamoto
Kosa la nane, kutokuwa tayari kupokea changamoto. Wakati mwingine
wajasiriamali wengi hushindwa kudumu katika biashara zao kutokana na
kutokuwa tayari kukubali changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika
shughuli zao za kila siku.
Ikiwa mmoja wa marafiki au ndugu anakwambia juu ya jambo ambalo si
zuri katika biashara yako yafaa kutopuuza. Kaa chini na ufanye tathmini
ya kile unachoambiwa kwani huenda kikasaidia kuokoa biashara yako juu ya
jambo fulani.
Kuambiwa jambo fulani juu ya biashara yako hasa usilopenda si
kwamba ukae katika nafasi ya kufanya kila wasemalo, bali jambo kubwa la
kufanya ni kusikiliza. Huwezi kujua kuna siku watakupa ushauri mzuri
zaidi wa kuboresha biashara yako.
Kosa kurudia kosa
Kosa la tisa, kosa juu ya makosa yote ni kurudia makosa yale yale
kila wakati. Makosa hayakwepeki na ni sehemu ya shughuli za
wajasiriamali kila siku. Tatizo linakuja kama utakuwa mtu wa kurudia
makosa yale yale kila wakati, utarudi nyuma tu.
Wajasiriamali wanapaswa wawe watu wa kujifunza kutokana na makosa
si tu wanayoyafanya bali hata yale wanayoyaona kutoka kwa wengine. Kama
utakuwa unajifunza kutokana na makosa, basi utakuwa na uhakika wa kuokoa
pia fedha zako.






0 comments:
Post a Comment