Yanga: Mbeya City angalieni tarehe 12

Author
Baada ya kuibuka na ushindi mkubwa dhidi ya Coastal Union juzi, Yanga wameitaka Mbeya City iangalie tarehe kwa kuwa idadi ya mabao wanayofunga kwa sasa hulingana na terehe ya siku husika.
 
Yanga, mabingwa mara 24 wa Tanzania Bara na wawakilishi pekee wa nchi waliosalia katika michuano ya kimataifa ya klabu mwaka huu, walitoa kipigo kikubwa cha mabao 8-0 dhidi ya Coastal katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ikiwa ni siku ya Jumatano Aprili 8.
 
Kikosi cha Mdachi Hans van der Pluijm, kitashuka Uwanja wa Taifa Jumapili Aprili 12, kuikabili timu iliyopunguza makali yake ya msimu uliopita, Mbeya City katika mwendelezo wa ligi hiyo huku uongozi ukitamba kuwa City itafuata nyayo za 'Wagosi wa Kaya' kwa kubamizwa mabao mengi.
 
Pluijm aliliambia NIPASHE mara tu baada ya mechi ya juzi kuwa mechi za VPL dhidi ya Coastal na City ni sehemu ya maandalizi yao kabla ya kuikabili Etoile Sportive du Sahel (ESS) katika michuano ya kimataifa.
 
Kutokana na kipigo cha mabao 8-0 kuangukia Aprili 8 (juzi), Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Yanga, Jerry Muro, alisema jijini jana kuwa City inapaswa kuangalia tarehe ya mechi yao inayofuata kisha ijiandae kupokea idadi ya mabao ambayo alitamba itakuwa sawa na tarehe husika.
 
"Coastal tumewafunga mabao 8-0 tarehe nane, Mbeya City kabla ya kututangazia vita sisi (Yanga), wanapaswa kuangalia tarehe ya mechi yetu dhidi yao. Tutawapiga mabao 12 Jumapili maana tuna wachezaji wenye uwezo huo. Yanga hii ni ya kimataifa. 
Wazitangazie vita timu za mchangani," alisema Muro.
 
Baada ya kuishika Azam FC kwa sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Azam jijini juzi na kuwagombanisha Meneja wa Azam FC, Jemedari Said na Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO), Saad Kawemba, kocha mkuu wa City, Juma Mwambusi, aliwataka wachezaji wake wajiandae kwa vita dhidi ya Yanga Jumapili.
 
Mwambusi, kocha bora wa VPL msimu uliopita, alisema: "Nashukuru wachezaji wangu wamepambana, tumepata  pointi moja ni jambo zuri kwetu kwa sababu tutakuwa tumesogea katika nafasi nyingine, tuna mchezo Jumapili, hivyo tujiandae na tujue kuwa tunatakiwa kuipigania timu yetu mpaka dakika ya mwisho."
 
Yanga iko kileleni mwa msimamo wa VPL ikiwa na pointi 43 baada ya mechi 20 wakati City iko nafasi ya saba ikiwa na pointi 25 baada nayo kushuka dimbani mara 21.
 
City imefungwa mara mbili dhidi ya Yanga katika mechi tatu walizokutana, na timu hiyo ya Jiji la Mbeya haijawahi kupata ushindi dhidi ya Wanajangwani hao tangu ipande Ligi Kuu msimu uliopita.
 

0 comments:

Post a Comment