Kama kuna mtu anayesema kuwa hana kitu cha kuandika basi
hajafikiri kwa undani au ni mwongo. Kila binadamu ana kitu chema ndani
yake. Ukishaandika vitu hivyo, angalia kama vitu vikifanywa na mtu baki,
usiyemjua je utasema yeye ni mtu mbaya?
Kama siyo, kwanini unajiona usiyefaa na uliyejaa
mabaya tu? Badala ya kutazama yale yaliyo mabaya na yakushindwa katika
historia yako, tazama mafanikio.
Kila mmoja ana mafanikio ya aina fulani, hata kama
ni madogo. Wengi wetu hatuchukui muda kujiuliza vyanzo vya mitazamo
yetu. Ila mara tu utakapogundua kuwa tatizo sio lako wewe bali ni
mazingira uliyokuziwa au aina ya wazazi uliokuwa nao, basi utaacha
kujidharau.
Wako watoto wanaofurahia kupelekwa shule za bweni mbali na nyumbani, ila wako ambao hawapendi kabisa, lakini wanalazimishwa.
Hali hii hupandikiza ndani ya watoto hawa, upweke,
hofu, msongo wa mawazo na kutokutulia (nazungumzia utulivu wa ndani)
jambo ambalo huendelea hata katika utu uzima wao.
Wako wengi ambao tabia zao za leo zilianza
kuharibikia katika shule za bweni mbali na wazazi kwa mfano tabia za
kusagana au kuingiliana kinyume na maumbile.
Sisi tumeumbwa katika mifumo na vipindi
mbalimbali, mara nyingine tuko chanya (watu wema, wazuri) na mara
nyingine tunakuwa hasi (watu wabaya). Kama mtoto atakuwa akiambiwa kila
wakati kuwa ‘kamwe huwezi kuwa na akili kama dada yako’ maneno haya
hufanyika halisi kwake.
Je hujawahi kusikia mtu akisema: “Mimi sijui
kuogelea”, “Sijui kama nitaolewa”, “Kamwe sitokaa niendeshe gari”, “Mimi
sitokaa nijue Kiingereza” na “Mimi na kuimba ni tofauti.”
Haimaanishi kama watu hawa wangeanza kujifunza au
kuzaliwa katika mazingira ya vitu hivi, wangevishindwa. Labda kuna
sehemu mtu au watu fulani waliwasemea kutoweza au kushindwa na huo ukawa
mwanzo wa kuwekewa kizingiti cha ujuzi ndani yao.
Wakati wowote mtu anapojisemea jambo au neno
lililo baya, lisilojenga, lakushindwa, kama utalisema kwa sauti au
utalifikiria akilini, katika hali yoyote ile jambo hili hulazimisha
uhalisi wa maneno yale kuingia katika mfumo wa maisha yako na kutenda
kazi kwa hiyo jifunze kukataa, kukanusha na jitahidi kutenda kinyume na
zile sentensi mbaya juu yako.
Kama tunaamini utendaji wa kazi wa yale
tunayojisemea au kusemewa vibaya basi hata yale tunavyojisemea au
kusemewa vema hutenda kazi pia.
Amua kubadilisha yale unayojisema au yale unayosemewa. Badili yale yaliyo hasi (yakufeli) yawe chanya (yakuweza).
Kama hujiamini wewe mwenyewe wala hujithamini, basi utakubali
kirahisi kila neno gumu, hutaweza kukabiliana na ushindani wa mtu au
watu wenye tabia ngumu.
Kumbuka daima udhaifu huanzia kwako mwenyewe.
Ukishajifunza kupunguza kujilaumu na kujipinga mwenyewe na kuboresha
jinsi unavyojitazama basi utakuwa salama katika kukabiliana na maneno na
matendo magumu toka kwa yeyote mwenye tabia ngumu.
Na kwa kuwa umejifunza vizuri kujielewa basi sasa
waweza kuwaelewa vizuri zaidi wale wenye tabia ngumu. Sasa utaweza
kuelewa kuwa kuna kitu kimemfanya au kimewafanya wawe vile walivyo.
Mara utakapoweza kumwonea huruma yeyote, haijalishi anatisha kiasi gani basi hawezi tena kukuathiri kwa vyovyote vile.
Kwa jinsi ujasiri wako unavyoongezeka, unaweza pia
kuziweka katika matendo mbinu nyingine nyingi za kushughulika na watu
wenye tabia ngumu.
Utajikuta unaweza kukabiliana nao na pia
kuchukuliana nao katika mazingira tofauti na pia hata katika nyakati
ambazo hutakuwa unafanya vizuri katika jambo fulani, hautajilaumu na
kujishusha, bali utajisifu kwa kukazana na kujitahidi hata kama
haukubahatika.
0 comments:
Post a Comment