wakamatwa na meno ya tembo

Author
Jeshi la Polisi mkoani  Katavi limewakamata watu wawili kwa tuhuma za kukutwa na meno ya tembo  vipande 22 vyenye uzito wa kilogramu  46 na thamani ya Sh157 milioni   wakati wakiyasafirisha kwa basi kutoka Mpanda  kwenda Mkoa wa Kigoma
Kaimu Kamanda  wa  Jeshi la Polisi wa Mkoa wa Katavi,   Rashid Mohamed aliwataja watuhumiwa hao Justine  Baruti (Zolros) (39) Mkazi wa Kijiji cha  Ivungwe makazi ya Wakimbizi ya Katumba Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi  na  Bonifaphace  Hoza (40) Mkai wa  Kalele Wilaya ya Kasulu  Mkoa  wa Kigoma. Alisema watuhumiwa hao walikamatwa na askari wa doria  juzi asubuhi katika eneo la stendi ya mabasi ya Mpanda.
 Mohamed  alisema askari hao baada ya kupekua mizigo ya mtuhumiwa  Justine walimkuta akiwa na meno  ya tembo  vipande 15  vyenye uzito wa kilogramu 33  vyenye thamani ya Sh90 milioni  sawa na tembo  wanne waliouawa vikiwa vimehifadhiwa  ndani ya  mabegi makubwa mawili.
Alisema  baada ya  Justine kupekuliwa na kukutwa na meno hayo ya tembo  mtu mwingine ambaye  inaonyesha  alikuwa na mtuhumiwa  alitupa begi lake la rangi ya ugoro na kisha kutokomea  kusikojulikana.
Mohamed alisema baada ya polisi kufanya  ukaguzi wa kina  kwenye basi walilokuwa wakisafiria watuhumiwa, walifanikiwa  kumkamata mtuhumiwa  Bonifaphace   Hoza  akiwa na begi moja  alilokuwa amelihifadhi  chini  ya  siti ndani yake likiwa na vipande  saba  vya meno ya tembo  vyenye uzito wa kilogramu  13 vyenye thamani ya Sh67,500,000 ambayo ni sawa na tembo  watatu waliouwawa.
 Alisema  watuhumiwa hao wawili  watafikishwa mahakamani  baada ya upelelezi kukamilika.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi waliozungumza na mwandishi wa habari hizi wamedai kuwa ipo haja kwa Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kuchukua hatua za makusudi ili kudhibiti biashara hiyo haramu ambayo baadhi ya watumishi wa Serikali ni wazi watakuwa wakishiriki kwa kuwa vitendo hivyo vimeshamiri na udhibiti wake kama vile umeshindikana mkoani humo

0 comments:

Post a Comment